Sunday, 23 December 2012

MTINDO WA MAISHA


TANZANIA  HIGHER  LEARNING  INSTITUTIONS  OF
SEVENTH  DAY
ADVENTIST  STUDENTS  ORGANIZATION(THISDASO).


“FUNGUA  MASIKIO”      Mithali 28:9

SOMO la 1.
MAWASILIANO.
Mawasiliano ni njia inayotumiwa na watu au viumbe hai vingine kupeana habari, mawazo au hisia mfano; mavazi, kuimba, machozi n.k
Mawasiliano ni neno pana na lenye kubeba mambo mengi mbalimbali katika nyanja tofautitofauti.
Mawasiliano katika maisha ya binadamu ni ya muhimu katika nyanja zote kiroho, kimwili, na kiakili.


MAWASILIANO NA  MUUMBAJI WETU.
·      Sisi kama vijana wa kiadventista, washiriki, wasomi na watu wote tunapaswa kujenga mawasiliano mazuri na Muumbaji wetu kwa kumtambua yeye ni nani? Na umuhimu wake ni upi kwetu.
Mfano: tunapaswa kuwa watu wa maombi ili uhusiano wetu uwe karibu na muumbaji wetu. Wafilipi 4:6, Luka 18:1

Wafilipi 4:6 “Msijisumbue kwa neno lolote, bali kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu.
Luka 18:1 “Akawaambia mfano ya kwamba, imewapasa kumuomba Mungu siku zote wala wasikate tamaa.

·      Kupitia mawasiliano, tunaaswa kumtukuza Muumbaji wetu na kumheshimu kupitia muonekano wetu, mavazi, usemu wetu, ulaji na mitindo yote ya maisha. Ili vijana wenzetu, watu wanaotuzunguka wapate kumuona Yesu na kujifunza kupitia kwetu.

1 Wakorintho 15:33 “Msidanganyike mazungumzo mabaya huharibu tabia njema”.
1 Wakorintho 10:31 “Basi mlapo, au mnywapo, au mtendapo. neno lolote fanyeni yote kwa ufukufu wa mungu.

MAWASILIANO NA WATU WANAOTUZUNGUKA.
·      Tunapaswa kuwa na mahusiano mazuri na watu wote bila kujali matabaka yaliyopo, elimu na kuona watu wote ni sawa na kumuona mwenzako ni bora kuliko wewe,ili iwe rahisi kuwapatia ujumbe wa HABARI NJEMA YA UPENDO WA MUNGU na tumaini la kurudi kwa Yesu mara ya pili kama utume wetu tulioitiwa.

Mathayo 28:19- “ Basi enendeni mkawafanye mataifa yote”kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba,Mwana na Roho mtakatifu”
Wafilipi 2:3 “Msitende neno lolote kwa kushindana wala kwa majivuno, bali kwa unyenyekevu,kila mtu na amhesabu mwenziwe bora kuliko nafsi yake”

·Kupitia mawasiliano,tunapaswa kuwakilisha msimamo wa imani yetu ya kudumu kuwa washiriki waaminifu katika usemi,mwenendo,usafi na imani ili watu wajifunze kupitia kwetu.

1Timotheo 4:12 “Mtu awaye yote asidharau ujana wako,bali uwe kielelezo kwao waaminio,katika usemi na mwenendo na katika upendo na imani na usafi”

Habari zote tunazotoa katika vyombo vya mawasiliano,zinapaswa kuwa zenye ukweli na zinazo mjenga msomaji,msikilizaji au mtazamaji na zenye kuhimiza imani ya dhati,utakatifu na ukweli.     

CHANGAMOTO
Ewe Mwanafunzi,mwanachuo uliyepo katika mazingira ya chuoni unatumiaje vyombo hivyo vya mawasiliano?Unawasiliana nini na wenzako kupitia vyombo hivyo? Kama; simuzamkononi,e_mail,face_book,twitter,lap_top na vyombo vingine? Je unawakumbusha wenzako mambo  ya kiroho kupitia vyombo hivyo,kujulisha upendo wa Yesu na kumweka rafiki yako karibu na msalaba wa Yesu?
Au unatumia vyombo hivyo kwaajili ya umbea,masengenyo,udaku,kutumiana meseji za mapenzi(uasherati&uzinzi) na mengine yafananayo na hayo?

 katika makundi tunayo soma(group discussions) ni ujumbe upi tunawapatia  wenzetu? Kumbuka tupo katika kipindi cha mwisho cha kuelekea kufunga historia ya ulimwengu.

Jihoji!!!...... Tafakari
Tunapaswa kujua uhuru wa kuwasiliana ukizingatia maadili ya mawasiliano,uwazi na uaminifu.
Hivyo waajiri,waajiriwa,wanachuo,wanafunzi na watu wote tunapaswa tujue uwazi,uwaminifu na kuwa na mahusiano ya karibu yenye kujenga.           

FAIDA ZA MAWASILIANO
1.Mawasiliano mazuri yanaweza kukufikisha katika mafanikio makubwa kwa kuwa na mahusiano mazuri kijamii na watu wengine bila kujali matabaka walionayo,utapata elimu kwa kubadilishana mawazo na kukua kitaaluma unapo jishirikisha na kujihusisha katika mashirika mbalimbali.

Mungu ametufunulia kutambua nyakati,ishara na matukio mbalimbali. Mfano: dalili za kurudi kwa YESU mara ya pili Mathayo 24:3-14.ishara ya upinde wa mvua baada ya gharika n.k.

Mwanzo 11:11 “Na agano langu nalithibitisha nanyi,wala kila chenye mwili hakitafutwa tena kwa maji ya gharika,wala hakutakuwa tena gharika,baada ya hayo kuiharibu nchi”
2.Mawasiliano yanatusaidia kudai ahadi zetu,dhidi ya wale tunao wasiliana nao.Mfano: kupitia maombi yetu na MUUMBAJI wetu tunaweza kudai ahadi zetu kwake.

Wafilipi 4:6 “Msijisumbue kwa neno lolote bali katika kila neno kwa kusali na kuomba haja zenu na zijulikane
1.Kupitia vyombo vya mawasiliano tunaweza kuvunja kwa MUNGU”

HASARA ZA KUTUMIA VIBAYA MAWASILIANO.
sheria ya MUNGU (amri kumi za Mungu)waziwazi.
Mfano:kusema uongo,umbea,kusengenya,kutamani,ufisadi,rushwa,kutumiana meseji za mapenzi(uzinzi&uasherati),kuangalia ponographical pictures na mengineyo.
Hali kama hii inapaswa kukemewa mara moja na kuepukwa  kabisa.

2.Upotevu wa mali nyingi kupitia vyombo hivyo bila kuona mafanikio yake.

3.Kuharibu ndoto au njozi za maisha yako,kushindwa kufika pale unapo takiwa kufika. Mfano: mimba zisizo tarajiwa,ndoa ambazo hazijapangwa au zisizotarajiwa.

4.Upotevu wa muda kwenye vyombo hivyo vya mawasiliano kama vitatumiwa vibaya hasa katika e-mail,facebook,twitter na vingine.

5. Mavazi na usemi wetu vyaweza kuondoa uwepo wa roho mtakatifu katika maisha yetu.Tunabaki bila roho wa Mungu,HASARA  ILIYOJE!!.
Wakolosai  1:10-11

WITO
 Tuendelee kudumu kuwa na mawasiliano mazuri na MUUMBAJI wetu,watu wanao tuzunguka katika makazi yetu(nyumbani)kazini na masomoni pia.TUTABARIKIWA.


                         Somo la 2.
KUTEMBEA KATIKA BARABARA YA UTAKATIFU USIO NA HILA.
Utakatifu maana yake ni kutokuwa na dhambi yoyote.ni kuwa mweupe na safi kabisa kwa kila jambo. Na Biblia inatueleza kwamba Mungu peke yake ndiye mtakatifu.

ZAB 99:9è”Mtukuzeni Mungu wetu; sujuduni mkiukabili mlima wake mtakatifu;        Bwana Mungu wetu ndiye mtakatifu.
Tunapaswa kumtukuza Mungu wetu na kumtolea ibada kwa kua yeye anastahili kuabudiwa nasi tu kazi ya mikono yake.

UFUNUO: 4:8 è”Na hawa wenye uhai wanne kila mmoja alikuwa na mabawa sita na  Pande zote na ndani wamejaa macho na wala hawapumziki usiku na Mchana, wakisema Mtakatifu Mtakatifu Bwana Mungu mwenyezi Aliyekuwako aliyeko na atakayekuja.
Hakika Mungu anastahili kuabudiwa.Kama viumbe walioko mbele zake hawachoki wala hawasinzii, ibada kwa Mungu ni masaa ishirini na manne na wala hawatoi udhuru, na wala hawakuanguka katika dhambi, lakini wanaishi kwa kumtukuza Muumba wao. Je wewe na mimi tunafanya hivyo? Viumbe wa mbinguni wanajua faida za kumtolea Mungu Ibada kama stahili yake!

ISAYA 57:15 è “Maana yeye aliye juu aliyetukuka akaaye milele  jina lake ni mtakatifu asema hivi.”Nakaa mahali palipoinuka palipo patakatifu, tena pamoja na yeye aliye na roho za wanyenyekevu na kuifufua mioyo ya watu”. Toba katika maisha yetu ni suluhisho la sisi kukubalika mbele za Muumbaji wetu 1Petro1:15-16 “Bali kama yeye aliyewaitwa  alivyo mtakatifu nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote kwa maana imeandikwa, mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu”.

 Vijana wa Kiadentista wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa mahali popote wawapo. Wajione kuwa wao ni mawakili wa siri za Mungu katika tabia na mienendo yao ili kanisa la Mungu lisitukanwe; Wajione kuwa wao ni wabeba nuru kati ya giza  la utandawazi unaoitumbukiza dunia katika tabia isiyofaa wala kumtukuza  Mungu wa mbinguni. Wajione kuwa wao ni hazina ya kanisa la Mungu popote walipo.Mungu huchukia dhambi hata wenye dhambi hawawezi kushirikiana naye ZAB 5:4,”Maana huwi Mungu apendezwaye na ubaya; mtu mwovu hatakaa kwako”.

ZAB.15:1-3 è “Bwana ni nani atakayekaa katika hema yako? Ni nani atakayefanya maskani yetu katika kilima chako kitakatifu? Ni mtu aendaye kwa ukamilifu na kwa kutenda haki. Asemaye kweli kwa moyo wake, asiyesingizia  kwa ulimi wake, wala hakumtenda mwenziwe mabaya, wala hakumseng’enya jiani yake”.Mungu wa mbinguni asiye na hila hutamani watu wawe mfano wa kuigwa ambao matazamio na makusudi yao ni kuishi pamoja na Mungu katika ufalme wake;
kuwa miongoni mwa watu hao”. Mungu alikataa kuwasaidia Waisraeli walipokuwa pamoja na wenye dhambi, yaani Akani mwana wa Karmi Yosh 7:1,10-12.

Watu wasiofaa wenye dhambi kama Akani wanaweza kuwa mzigo kwa ndugu,dada na wanaosafiri safari ya matumaini. Lakini mmoja wetu aweza kuwa kikwazo cha Mungu kutokuwa  upande wetu. Je,wewe ni Akani utabishaye kundi hata Mungu hataki kusikia maombi yetu?

Mungu hutoa mwito kwetu leo 2 kor 6: 17- 18 “Kwa hiyo tokeni kati yao mkatengwe  nao asema BWANA, msiguse kitu kilicho kichafu,nami nitawakaribisha, nitakuwa Baba kwenu nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike asema Bwana Mwenyezi.”

Tunatakiwa tumwone Mungu katika maisha yetu ya kila siku.Naamini  hatutabaki kama tulivyo. Musa aliomba aonyeshwe utakatifu wa Mungu Kut 33:18-23.
Mungu alikuwa tayari kumwonyesha utukufu wake kwa sharti la kumficha kwenye mwamba ili asidhurike.  Tutakapotamani kukaa pamoja na Mungu, Mungu yuko tayari kutuficha katika mwamba wake, yaani Yesu kristo  atatufunika kwa haki yake ili tustahili kusimama pale.

Isaya alipomwona Mungu akaona mapungufu  yake akatamani kubadilishwa ili akubalike mbele zake. Mungu alikuwa tayari kumtuma malaika kwa ajili ya huduma kumtakasa. Vivyo hivyo nasi Mungu yuko tayari kwa ajili ya kubadilisha mielekeo yetu miovu kwa njia ya utakaso Isaya 6:1-5.

Mungu ni mtakatifu na utakatifu usio kuwa na hila wala hitilafu yoyote.Imetupasa  Sisi kukiri kwamba ndivyo alivyo, na tena hatuwezi kumkaribia tusipotakaswa Maovu yetu kwa njia ya kumkubali Yesu Kristo pale msalabani kama mbadala  kwa ajili ya dhambi zetu.
kwa nini usitoe maisha yako kwake ili utembee katika barabara ya utakatifu usio na hila?
Kusudia moyoni mwako tangu sasa.


SOMO la 3.
MUNGU ANAYEJALI
-      Wana wa manabii ambao walikuwa katika shule za manabii walikuwa wakikaa pamoja.Na Mungu alikuwa akiwafunulia mambo ambayo alipenda wayafahamu. 2Wafalme 2:3-4

-      Hapa tunawaona Eliya pamoja na Elisha. ”Elisha akasema kama Bwana aishivyo na roho yako iishivyo sitakuacha:Basi wakashuka mpaka Betheli:Basi wana wa manabii walio kuweko Betheli wakamwambia Elisha: Je unajua kuwa BWANA atamwondoa bwana wako leo asiwe mkubwa wako?”
Wana wa manabii ambao walikuwako Yeriko walifahamu jambo hili la kuondolewa ELIYA.-soma 2Wafalme 2:5.       
      
HEBU TUANGALIE KISA KUTOKA KWA WANA WA MANABII.
2Wafalme 6:1-7.
Fungu la 2Walme 6:3- Mmoja wa wana wa manabii akasema “Uwe radhi,basi nakusihi uende pamoja na watumishi wako.”Akajibu nitakwenda.
·      Kazi ya kukata miti ya ujenzi ilianza lakini akatokea mmoja wapo wa wale watoto wa  manabii shoka yake(boriti) ilizama katika maji. 2Wafalme 6:5.

Mambo yaliyo mpata baada ya kupoteza ile shoka:-
®   Hofu na mashaka vilitawala moyo wake.
®   Hakujua namna ya kuweza kuitoa katika maji.
®   Shoka ilikuwa ni ya kuazima. Angesema nini juu ya mwenye shoka? 2Wafalme 6:5b.
®   Alisahau kuwa alikuwa na mtumishi wa Mungu.
Mungu anaye jali aliyaona yote yaliyo msumbua huyu kijana.Ndipo roho wa Bwana akamtumia nabii Elisha, “kilianguka wapi…?”,Akamwonyesha mahali.Akakata kijiti akakitupa palepale chuma kikaelea.    2Wafalme 6:6

Ni fundisho gani tunalipata katika kisa hiki?
(a). Mungu alijishugulisha na mkasa wa kukitoa chuma cha boriti ya shoka kupitia kwa mtumishi wake Elisha
(b). Mungu wetu yuko tayari kusikia hitaji la kila mmoja wetu,hajali kuwa wewe ni mtu wa namna gani.
(c). Wana wa manabii walikuwa tayari kusikia na kutekeleza kile alichosema Nabii 2Wafalme 9:1-6
(d). Wana wa manabii wakiwa katika shule na vyuo vya manabii walijifunza neno la Mungu, hata kutabiri.
{GILGALI, BETHELI NA YERIKO: 2Wafalme 2:3,5,15, 4:38}

MASWALI YAKUTAFAKARI
(i)        Je sisi tunaojiita Wakristo, tuko tayari kuongozwa na Roho Mtakatifu?
(ii)      Misingi ambayo Mungu aliiweka kwa manabii wake imetuonyesha jinsi wana wa manabii walivyojihusisha na neno lake, pia kumtegemea. Je sisi wana vyuo, misingi ya vitabu vya neno la Mungu tunaisimamia vyema?
(iii)     Je imani yako leo imejengwa kwa nani?
(iv)      Neno la Mungu linasema inunue kweli wala usiiuze Mithali 23:23
Je umeinua kweli? Yaani maandiko matakatifu unayasoma na kuyafanya kuwa taa yako ya Maisha?. Zaburi 119:105
WITO.
Iwapo mungu akijali chuma kilichopotelea majini na kuweza kutenda mujiza kikaelea,mungu huyo pia anajali maisha yako,anajali elimu yakounapoyaamini maandiko matakatifu.
2 Timotheo 3:16-17

ASANTE MUNGU WETU ANAYEJALI AKUBARIKI”.

SOMO la 4.

MWADVENTISTA NA MTINDO WA MAISHA KATIKA MAZINGIRA YA CHUO.

Fungu kuu Warumi 12:1-2

UTANGULIZI.
Lengo la mada hii ni kuibua mjadala mpana katika kile kinachoitwa mtindo wa maisha na athari zake kwa maisha ya vijana waadventista wa Sabato chuoni, hivyo kwa kifupi,mada chache tu katika eneo hili zimeguswa kama kichokoo kutupeleka katika mjadala wa kina dhidi ya mada hii.

Mtindo wa maisha (life style) ni jumla ya mambo yote yanayohusiana na namna ya ulaji, unywaji, matumizi ya pesa, mavazi na uvaaji, matembezi (outings), muziki, matumizi ya vyombo vya mawasiliano kama;simu za mkononi, ipod, runinga, tovuti, Email n.k katika maisha ya kila siku ya  familia au jamii.

Nukuu: According to www.businessdictionary.com/definition/lifestyle “Lifestyle is expressed in both work and leisure behavior patterns and (on an individual basis) in activities, attitudes, interests, opinions, values, and allocation of income. It also reflects people's self image or self concept; the way they see themselves and believe they are seen by the others. Lifestyle is a composite of motivations, needs, and wants and is influenced by factors such as culture, family, reference groups, and social class.

Kuna changamoto kubwa sana katika ulimwengu wa leo,hususan tunapozungumzia dhana ya mtindo wa maisha. Suala hili halikomei katika kuajadili kumomonyoka kwa maadili peke yake, bali pia hugusa kwa kiwango kikubwa wajibu wa kiroho kwa kila mmoja wetu, kwani athari zake zinaonekana wazi katika maisha yetu.

Inaonekana dhahiri kuwa, mitindo ya maisha inazidi kuleta athari kubwa za  kimwili, kiakili na kiroho   kwa vijana wetu hususan walio katika taasasi za elimu ya juu, hasa vyuo vikuu na vyuo vya kati. Hali hii inachangiwa kwa kiwango kikubwa na upanukaji wa mawasiliano yaliyopelekewa na kutapakaa kwa utandawazi ambao kwa namna moja au nyingine umeleta athari kubwa  za kiuchumi, kisiasa, na kijamii hivyo kuathiri mtindo wa maisha na kusababisha vijana wetu kujaribu kupambana na athari zake  kwa kuiga mitindo ya maisha ya magharibi amabayo kwa namna moja inaonelewa kuwa ndio mitindo bora ya maisha kwa makundi rika yaliyo mengi duniani.

 MTINDO WA MAISHA YA ULAJI NA UNYWAJI.
1Wakorintho 10:31,Mithali 16:3, Mithali 20:1,
Danieli,Shadrack, Meshack na Abedinego (Dan 2-3), Musa na Yusufu wanabaki kuwa kielelezo bora cha wasomi wa kale waliofanikiwa sana katika kumtetea Mungu wakiwa ndani ya taasisi mbalimbali za kielimu na utumishi katika nchi za ugenini.Haikupata kutokea wakaathiriwa na mitindo ya maisha kiasi kwamba wakamwacha Mungu na kugeukia anasa kama vijana wetu leo.

Ni dhahiri kuwa, baadhi ya vijana wetu katika vyuo vya elimu ya juu na kati, wamedhihirika kushiriki sana ulaji wa vyakula najisi pamoja na unywaji wa vileo mbalimabli kama vile bia,(beer) na vingine vinavyo sisimua miili yao,(Counsels on health pg450) Mambo haya yamechangia kwa kiasi kikubwa vijana wa aina hiyokukwepa sana kujiunga na vyama vya vyuo kama THISDASO mara wanapoingia chuoni. Matumizi haya ya anasa na vyakula najisi pia hudhihirika katika shughuli za mahafali pale vijana wetu wanapohitimu masomo yao, mambo haya hufanyika kwa siri katika kumbi za starehe au katika mahoteli na migahawa ya kisasa,(selected messages vol.3 pg 287, Patriarchs’ and Prophets pg562). Hali hii huchukuliwa na wanafunzi kama kiwango cha juu cha ustaarabu na usasa. Kuzoelea anasa huku kumehafifisha sana makuzi ya kiroho kwa vijana wetu walio wengi ambao kwa taaluma zao,wanatarajiwa hapo baadaye kushika nyadhifa mbalimbali za kanisa ili kulivusha katika changamoto kubwa hizi za maisha ya kiroho,kimwili na kiakili. Je wewe ni mmoja wao na ni hatua gani unachukua kukabilina na changamoto hii?

MTINDO WA MAISHA, MAVAZI NA  MATUMIZI  YA PESA.
1Timotheo 6:10,Mathayo 6:22-23
Matumizi ya anasa yamesababisha vijana walio wengi kutamani pesa kwa kiwango kikubwa, hali hii imekumba vijana wetu walio wengi. Pesa imekuwa chanzo cha vishawishi vingi hususani ngono, ulevi, ulafi, mavazi ya garama na anasa za matembezi yaitwayo(outings) pamoja na (picnics) ambayo yamechochea mazoea ya U-Boy friend na U-girl friend unaoishia katika mimba zisizotarajiwa au kuaibishana na kudhalilishana kwa wapenzi hawa ambao hawakutarajia ndoa hizo za mapema.
Pesa imekuza uadui baiana ya mtu na mtu na imechochea,chuki,husuda,kijicho,umbea,unafiki,wivu,mauji,magonjwa kama UKIMWI na kukosa subira. Na Kwa jinsi hiyo wengi wamenaswa katika mtego wa yule mwovu kiasi cha kushindwa kusimama imara juu ya mwamba ambaye ni kristo.Imani wameiacha na kujikuta wakiwa mawakala wa shetani katika mazingira ya vyuo vyao. Nijukumu la vijana wetu kutambua kuwa kutamani pesa sana kuna leta athari kubwa kwa maisha ya kijana mwadventista. Yatubidi kuwa na kiasi na kutambua uwezo wetu. Si vyema kutamani matumizi  ya pesa yanayozidi kiwango cha kipato chetu kwani madhara yake ni makubwa mno katika maisha yetu. Chukua hatua jifunze madhara ya pesa kupitia kisa cha YUDA ISKARIOTE. 

Lakini pia mitindo ya mavazi ya kimagharibi kama vile uvaaji wa suruali kwa mlegezo au (KK) kama inavyojulikana,sketi za kubana, vi-body, vi-top, stretcher-trouser, mitindo ya kusuka nywele na matumizi ya Mecuric-creams au Mikorogo kwa ajili ya kuchubua ngozi vinazidi kushika kasi kwa vijana leo kanisani.Hali hii haiwezi kuachwa tu bila ya kukemewa na kanisa, hasa pale kanisa linapo jiaandaa kumlaki Bwana Yesu hivi punde. Tamaa hizi mbaya lazima zionywe kwa neno la Mungu (Evangelism pg 272, Child guidance 429,430). Aina hii ya mavazi na uvaaji ni lazima ipigwe marufuku katika makusanyiko matakatifu. Vijana wasaidiwe kwa hekima kuona ubaya wa mivuto hii isiyokubaliana na imani yetu.

MTINDO WA MAISHA NA MATUMIZI YA MUZIKI NA VYOMBO VYA MAWASILIANO.
Warumi 8:4-8
Katika Nyanja ambazo shetani amejipatia wateja wengi leo ni hii ya muziki na vyombo vya mawasiliano.Leo muziki umekuwa mojawapo ya mahitaji ya msingi ya binadamu.Katika kizazi hiki,muziki, hasa ule wa kimagharibi umekuwa ukitukuzwa na kuingizwa katika baadhi ya ibaada za madhehebu ya kikikristo, lakini pia si ajabu tamaduni hizi za kishenzi zimaenza kupenyezwa hata ndani ya kanisa la Mungu,inatubidi kuchukua tahadhari kubwa tunapo chagua nini cha kusikiliza.(Education pg 167-168, Testmonies vol 4,pg 652-653)

Isitoshe leo kunavijana wetu wa kiadventista wanahudhuria katika kumbi kubwa za muziki na kukesha huko wakimtumikia mwovu,mazoea haya yameathiri tabia zao njema na kuua imani na uhusiano wao na Kristo Yesu.

Hata hivyo matumizi ya simu za mikononi, laptop na tovuti ni mojawapo ya mitindo ya maisha inayoleta madhara makubwa kwa vijana wetu. Tovuti badala ya kuwa vyanzo vya taarifa za masomo, vijana wetu walio wengi wamekuwa wakivitumia kama njia ya kujifunza mambo machafu ya ngono ambayo yanaathiri sana mwelekeo wao maisha ya baadaye hususani katika maisha yao ya ndoa(1 wakorintho 6:8).
 
Vivyo hivyo simu za mikononi nazo pia zinatumika kwa makusudi kama hayo ikiwa ni pamoja na kupashana ujumbe wa mapenzi au kuchochea ashiki za kingono. Mambo haya yasipoepukwa hayatamwacha salama kijana mwadventista.Mkazo uwekwe kwa kiwango kikubwa katika kusimamia na kuhamasisha vijana wetu kuishi maisha matakatifu yanayompendeza Mungu

WITO.
Wakati umefika kwa vijana wetu kuamka katika usingizi wa kiroho na kupambana na hali hii mbaya inayodhoofisha ukuaji wa kiroho kwa vijana wetu. Tukiwa wasomi katika taaluma mbalimbali ni vyema basi tutumie elimu zetu kwa uangalifu huku tukimwinua Yesu juu kupitia maisha yetu ya kimwili,kiakili na kiroho.Nikujidanganya bure kudhani kuwa unajua unachokifanya,Bwana anonaye sirini ataleta kila jambo hukumuni liwe jema au liwe baya.Wapo wengi wenye hekima na wasomi waliobobea katika Biblia ambao walidumu kumcha Mungu pamoja na hadhi zao,na Bwana aliwainua juu sana na kuwakweza kama alivyotenda kwa Musa pale Misri. 

Kama kijana Mwadventista unapaswa kuwa kielelezo ndani ya kanisa,ndani ya maeneo ya chuo chako, katika kundi lako la kujisomea, na jamii kwa ujumla, jihadhari kumtweza roho wa Mungu pale anaponena nawe leo.
Chagua kufanya matengenezo ya kweli.


SOMO LA 5.
KIOO CHA AJABU.
(SHERIA YA MUNGU ISIYOBADILIKA)
FUNGU KUU: “Sheria ya BWANA ni kamilifu, huiburudisha nafsi, Ushuhuda wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima”. Zab 19:7
Ni jambo la pekee na lenye faida kubwa kuwa,mtu aishikaye sheria ya Mungu anakuwa ni mwenye amani, furaha na mwenye uhakika wa kuuingia mji mtakatifu – Mbinguni.

Twaweza kujiuliza nini maana ya sheria………….?’

Sheria ni utaratibu, agizo au mwongozo wenye mamlaka uliotolewa na mwenye mamlaka kwa ajili ya kutoa maelezo sahihi kwa jamii katika kuelekeza, kusimamia, kukosoa na kuadibisha.
Sheria ya Mungu inafananishwa na kioo kwa maana hii kuwa,ina uwezo wa kuonyesha bayana / kwa usahihi uovu au makosa ya mwanadamu. Kwa sababu sheria yake ni kamilifu, inaonesha kwa usahihi usiokuwa na shaka yoyote kuwa dhambi ni hii na utakatifu ni huu. Yakobo 1:23, Warumi 2:13

Ila sheria yenyewe haina uwezo wa kuondoa dhambi/makosa – kama kioo kilivyo.
Maneno haya: sheria, Amri na torati katika maandiko matakatifu (Biblia) wakati mwingine hutumika katika ulinganifu au kwa maana sawasawa.
 Mfano. Soma aya hizi; Zab. 19:7, 1Yoh 5:3, Rum 7:7, Zab1:2, Yoh 14:15.

KAZI ZA SHERIA
Ndugu zangu wapendwa ninapenda tufahamu kuwa sheria ya Mungu ina kazi hizi zifuatazo (japo waweza kufahamu ngingi zaidi);
1.  Kuifanya dhambi ionekane/kuitambulisha dhambi. Rum 7:7-13
2.  Kutuongoza kwa Kristo (Sheria ni kiongozi) Gal. 3:24

SHERIA NA NEEMA
Ni kweli kuwa tunaokolewa kwa neema, ambayo hutuongoza kuikataa dhambi. Na hatuwezi kuitambua dhambi pasipokuwa na sheria.Naam, sheria huionesha/funua  dhambi  na Neema ya Kristo huiondoa. Tito 2:11-12.
MAKUNDI YA SHERIA
Katika Biblia, sheria yaweza kufundishwa katika namna nyingi au makundi tofautitofauti.
Hebu tuyatazame makundi makuu haya mawili.
(1). Sheria zilizoandikwa na Mungu, muumba wa mbingu na nchi.
(sheria/amri 10 za Mungu)
(2). Sheria zilizoandikwa na Musa, Nabii wa Mungu
(sheria za maagizo).

(1).SHERIA ZA MUNGU (Amri 10)

Hii inaitwa sheria ya Mungu isiyobadilika kwa sababu, Mungu habadiliki badiliki, yaani hana kigeugeu, na maneno yake ni amini. Hes. 23:19, Yak 1:17, Tito 1:2 na 1Sam 15:29

Sifa za sheria za Mungu.
(i)        Ziliandikwa na Mungu mwenyewe kwa chanda chake.Kut.24:12, 31:18, Kumb. 9:10
(ii)      Ziliandikwa katika mbao mbili za mawe Kut. 31:18
(iii)     Zilitunzwa ndani ya sanduku la agano. Kumb. 10:1-2
(iv)      Nakala ya sheria hiza iko mbinguni. Uf. 11:19
(v)       Zitatumika katika hukumu siku ya mwisho.

Ndizo zitakazokuwa kipimo katika hukumu ya Mungu ijayo
·      Yak 2:10-12 - Tutahukumiwa kwa sheria ya uhuru
·      Math. 19:16-19 – Ukitaka kuingia mbinguni, zishike amri
·      Rum 2:13 – Zishike amri.

“Watakaoingia mbinguni ni wale tu wayafanyao mapenzi ya Mungu,na mapenzi ya Mungu ni kuzishika amri zake. Mith. 7:20, Yoh 14: 15”.

(2).SHERIA ZA MAAGIZO
Kwa uongozi wa roho mtakatifu, sheria hizi ziliandikwa na Musa,na zina sifa hizi:
(i)        Mwandishi wake ni Musa (Nabii wa Mungu)
Kumb 31:9
(ii)      Ziliandikwa katika chuo/magombo/magome ya miti yaliyotengenezwa kwa ustadi. Kumb. 31: 24
(iii)     Zilihifadhiwa kando ya sanduku la agano lililokuwa na amri kumi (10) za Mungu. Kumb. 31: 26.

Sheria za maagizo zilihusu mambo haya:
(a). Tohara (Mwanzo 17:9-11)
Sheria hii ilifikia ukomo wake, kwani ilikuwa ni mfano kivuli. 1Kor. 7:19, Rum 2: 28-29
(b). Kafara ya wanyama (Walawi 16:15)
Sheria hii ilifika ukomo pale msalabani kwa sababu ya kafara ya Yesu Kristo, Luka 23:44, 45, 1Yoh. 1:7, Rum 5:9, 1Pet 1:19
(c). Ndoa (Walawi 18:20-22)
Sheria hii inaendelea. Ebr. 13:4, Kut. 20:14
(d). Mavazi (Kumb. 22:5)
Sheria hii inaendelea. 1Tim 2:9
(e). Afya (Walawi 11, Kumb.23:12-14)
Mungu anahitaji tule kilicho chakula (walawi 11) na kuyaweka mazingira safi (kumb. 23:12-14)
Sheria hii inaendelea. (1Kor.3:16-17, 6:19-20
(f).  Zaka na sadaka (Walawi 27: 30-34)
Twapaswa pia kulitekeleza agizo/ amri hii. Malaki 3:10
(g). Sikukuu (Walawi 25)
Ziko sikukuu zilizofikia ukomo na zingine zinaendelea. Mf. Isaya 66:22-23, kut. 31:12,17, Ezek 20:12, kumb. 16:13-19, Zek. 14:16

SHUGHULISHA UBONGO:
Rafiki wasafiri wenzangu, napenda tufahamu jambo hili kuwa, kuikataa sheria ya Mungu ni kuukataa mpango mzima wa wokovu
Hebu tazama kielelezo hiki:
(1). Sheria
(2). Dhambi
(3). Mhubiri
(4). Injili
(5). Mwokozi          
(6). Kanisa
(7). Wokovu

“Pasipo SHERIA hakuna DHAMBI (Rum 7:7). Na kama hakuna dhambi, hakuna hitaji la MHUBIRI/WAHUBIRI maana wao huihubiri INJILI inayomhusu MWOKOZI (Yesu Kristo) anayeikataa dhambi.
Watu wanapoisikia injili na kumpokea mwokozi huja KANISANI wakifanywa tayari na kujiandaa kuupata WOKOVU”.

HITIMISHO.
Watu wengi leo wanafanya jitihada za kila namna kutii sheria za wakubwa wao wa kazi, waajiri wao ama wasimamizi wao wenye mamlaka. Sheria hizi zinazingatiwa sana na kupewa heshima na nafasi kubwa.
Mfano. Wanafunzi shuleni au vyuoni, huzingatia sheria za vyuo ili wasifukuzwe vyuoni. Huzingatia sheria za mitihani kama; kuwa na kitambulisho cha mtihani, kuwa na vifaa vyote vya mitihani na hata vya ziada,kutokuwa na/kuto kukutwa na chanzo chochote cha majibu mf.karatasi(Nondo) n.k.
Kwa nini tusitie bidii kuzishika amri za Mungu wetu, tena kwa kutetemeka? Je Mungu si zaidi sana ya wanadamu hao tunaowaogopa kwa kuzizingatia sheria zao……….?“Tafakari ………………………!!

WITO:
Hebu ikubali sheria ya Mungu:
Tusipozingatia amri za Mungu, Kweli haimo ndani yetu hata kidogo 1Yoh 2,4 pia Sala zetu ni chukizo. Mith 28:9.

SOMO LA 6.
KWANINI UAMSHO WA KISASA HAUJAFAULU..?
Neno Uamsho ni neno zuri linaloleta maana halisi ya mpango wa kumwokoa mtu aliyekwama mahali Fulani kiroho, mtu ambaye kamwe hawezi kujikwamua bila kupata msaada toka nje ya uwezo wake.

 Mada hii kiasili imekuwepo tangu mwanadamu alipoanguka na kama ingetokea kwa bahati mbaya kizazi fulani kipite bila wacha Mungu kufanya Uamsho kwa msaada wa Mungu wao, basi kizazi hicho kingelipita bila Mungu kujipatia watu wake, na Mungu angaliweza kudharauliwa milele.

 Maneno haya yanaonyesha kwamba mtu wa kwanza kushikilia jukumu hili na kufanyia kizazi chake Uamsho mkubwa-alikuwa ni Adamu.
-          Kwa muda wa miaka karibu Elfu moja Adamu aliishi miongoni mwa watu akiwa shahidi  kwa matokeo ya dhambi, alikuwa ameagizwa kuelekeza vizazi vyake vijavyo katika njia ya Bwana na kwa uangalifu alitunza kile ambacho Mungu alikuwa amedhihirisha  kwake,na alikirudia kwa vizazi vilivyofuata kwa watoto wake, wajukuu zake hadi kizazi cha tisa alieleza hali ya furaha na takatifu ya mwanadamu katika paradise.Alirudia historia ya anguko lake akiwaelezea njia za huruma kwa ajili ya wokovu wao, na bado ni wachache tu walijali maneno yake. Mara nyingi alikutana na Malaumu kwa dhambi ambayo ilileta shida kama hiyo kwa vizazi vyake vijavyo.  (Patriaches&Prophets. uku 82 aya II).
         
Nabii anadhibitisha jinsi adamu alivyokuwa mwaminifu katika kufanya uamsho lakini pia anataja majukumu aliyokutana nayo  na hii ndiyo shida inayokikuba kizazi cha leo. Watu wa kizazi cha Adamu pamoja na kukataa Ukweli wa uwazi uliokuwepo wazi mbele yao na Adamu mwenyewe, lakini bado walikuwa hawajafikia mambo makubw a ya ubunifu tunayoshuhudia leo. Ukiachilia mbali Elimu tuliyonayo, leo makanisani huwezi kuamini kwamba ni mahali panapotajwa jina takatifu la BWANA yeye ambaye tunajifunza kwake kwamba kila kitu kilitoka mikononi mwake wala pasipo yeye hakikufanyika chochote kilchofanyika Yohana 1 : 1 – 4.

Yeye ambaye viumbe vitakatifu ambavyo havikuanguka vinamwabudu kwa hicho usiku na mchana bila kukoma na makerubi wakifunika nyuso zao kwa mabawa yao,Ufunuo 4 :8-11. 

 Huyo sisi tumemfanyia Uamsho wa bandia tukitumia jina hilo hilo takatifu,tunacheza  na kubakia uchi tunashangilia kwa makofi na vigelegele, tumeshuhudia hata vuvuzela kwenye baadhi ya nyumba za ibada,…….. ajabu ilioje!!

Tunachohitaji  kutafuta hapa ni,  kwa nini Uamsho wa kisasa unashindwa kufaulu?
 Kama hapa tungalikuwa na muda wa kotosha tungaliweza kuzama na kuangalia kizazi hadi kizazi tuone ni wapi walipofanya vibaya nani wapi walipofanya vizuri lakini wewe  kama mshiriki na mwanafunzi binafsi unao muda wa kutosha kufanya hayo yote, na zaidi hebu usilale, fanya kitu katika zamu yako. Habakuki 2 :1 -2

Kanisa la Mungu duniani limepewa jukumu zito la kuhakikisha kila anayeitwa mwanadamu ameambiwa habari  juu ya wokovu wake na kama anazo habari hizo tayari anaamshwa kundelea na safari.
Bila kufanya hivyo wengi watachanganyikiwa katika kizazi hiki lenye ukaidi ambapo kuna dhana mbalimbali ikiwemo dhana potofu inayo ila Dunia sasa hivi- dhana ya upako ambayo Inabeba mambo mawili makubwa ndani yake;

 Moja uponyaji na ya Pili utajizisho. Mambo ambayo kiasili hayakataliwi na maandiko  lakini adui ameazimia kutumia mambo  haya kama ndoano na Hakika  amefaulu na kuwanasa walio wengi.

Ukweli ni kwamba wote katika vipindi vyote waliyofanya Uamsho wa kufaulu walijitenga mbali na mambo haya yote wakatambua  dunia ya wakati wao, wakamweka Mungu kuwa  wa kwanza katika mambo yao yote.
·         Mwanngalie Yusufu kule misri ,
·         Mwone Danieli na wenzake wakiwa kule Babeli ,
·         Mwone Yeremia akisimama peke yake katika wakati  mgumu
·         Vipi Eliya mitishbi wakati wa ibada ya Miungu!

Tuwaone wanafunzi walioishi katika kipindi kigumu  cha utawala katili wa Rumi, walihitimisha historia kwa ushindi mkuu wakimwinua Kristo mfufuka  hata kama kama walikatazwa kufanya hivyo.

Kazi imebakia kwetu lakini Hatuwezi kufanya hivyo kama Hatutakubali kuondoa tofauti zetu na kuungana na kuwa wa sauti moja.Mkulima akifanya sehemu yake, mfanya biashara naye katika biashara yake, Mwanachuo naye kama Mwanachuo kwa sehemu  yake.

Kumbuka mwanachuo- kama Musa kwenye Ikulu ya Farao, Mungu amekaa kimya anasubiri kuona unamwakilishaje hapo ulipo, na hata wakati mwingine unalazimika ushuke kwenda kuwaangalia watu wako wanaoteseka, hiyo ni sehemu ya uamsho.

Bwana atakuwa msada wako-Uamsho wako utafaulu nawe utabarikiwa.
“Shuka sasa shuka leo Uwaone”.
Amina.
        “MARANATHA…..!!!”

No comments:

Post a Comment